Rais Magufuli: Hakuna Hela ya Bure katika Utawala Wangu, Lazima Watu Wafanye Kazi,,

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amefunguka na kusema  katika wakati wake hakuna kupata pesa kwa njia rahisi kwani lazima ufanye kazi kweli ili kupata pesa halali.

Rais Magufuli amesema hayo leo Handeni wakati anaelekea mkoani Tanga kwa ajili ya uwekaji wa jiwe la msingi mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Hoima nchini Uganda mpaka Chongoleani Tanga. Utaofanyika siku ya Jumamosi ya tarehe 05 Agusti mwaka huu.

"Kuna watu walikuwa wamezoea vya bure wanapiga 'disco' tu wanapewa hela nyingi hazipo pesa za namna hiyo, hivi sasa watu wanataka ufanye kazi uzalishe mali ili upate fedha za kweli na asiyefanya kazi asile na usipokula maana yake ufe" alisisitiza Rais Magufuli

Mbali na hilo Rais Magufuli amesema uchumi wa Tanzania unakuwa kwa kasi kubwa na kudai kwa Afrika katika nchi tano ambazo uchumi wake unakuwa kwa kasi kubwa Tanzania pia ipo imeshika nafasi ya pili nyuma ya Ethiopia.

"Ikiwa uchumi wetu unakuwa kwa asilimia 7.2% wapo watu watakuja na kulalamika hela zimepotea, hao walikuwa wamezoea vya bure, na hao ndiyo mnawaona wanapiga kelele" alisema Magufuli.

Kwa mujibu wa benki ya Dunia katika nchi ambazo uchumi wake unakuwa kwa kasi kubwa Tanzania imekuwa nafasi ya tano chini ya India, Nepal, Uzbekistan na Ethiopia ambayo ndiyo imekamata nafasi ya tano.